Watu zaidi ya milioni 3 walifariki kutokana na matumizi mabaya ya pombe
mwaka 2016. Zaidi ya robo tatu ya vifo hivi vilikuwa ni vya wanaume. Kwa ujumla,
matumizi mabaya ya pombe husababisha zaidi ya asilimia 5 ya mzigo wa magonjwa
duniani. Hii ni kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Shirika la Afya
Duniani (WHO) September mwaka huu ya ripoti ya hali ya Duniani kuhusu
unywaji pombe na afya 2018 (Global status report on alcohol and health
2018).
Kwa vifo vyote vinavyotokana na pombe, asilimia
28 vilikuwa vinatokana na majeruhi, kama vile ajali za barabarani, kujidhuru
na unyanyasaji wa kibinafsi, huku asilimia 21 vikiwa ni kutokana na
matatizo ya utumbo, asilimia 19 kutokana na magonjwa ya moyo, na sababu
nyingine ni kutokana na magonjwa ya kuambukiza, kansa, matatizo ya akili
na hali nyingine za afya.
Vifo vinavyotokana na matumizi ya pombe ni vingi
zaidi kuliko vile vinavyosababishwa na magonjwa kama vile kifua kikuu, VVU /
UKIMWI na ugonjwa wa kisukari. Kwa mujibu wa WHO mzigo wa maradhi ya pombe ni
mkubwa zaidi katika nchi za kipato cha chini (Tanzania ikiwemo) na kipato
cha kati ikilinganishwa na nchi zilizoendelea.
Matumizi ya kila siku ya watu wanaokunywa pombe
ni gramu 33 za pombe kwa siku moja, sawa na glasi 2 ya wine, au
chupa kubwa ya bia. Kwa ujumla, matumizi ya pombe
yanasababisha zaidi ya magonjwa 200.
Licha ya madhara ya afya, matumizi mabaya ya
pombe huleta hasara kubwa kijamii na kiuchumi, kwa watu binafsi na jamii
kwa ujumla.
Matumizi ya pombe na athari zake ni tatizo
linalozidi kukua nchini Tanzania, na linapaswa kudhibitiwa haraka iwezekanavyo.
TAAnet inazikumbusha taasisi husika pamoja na Serikali kuangalia kwa
hakara namna ya kudhibiti tabia hiyo ili kunusuru maisha ya vijana
yanayoendelea kuharibika kila siku. Kutokana na madhara makubwa ambayo yamekuwa yakisababishwa
na unywaji pombe, kama vile ilivyofanya katika kupinga matumizi ya viroba na
upatikanaji wa pombe nyingine rahisi.
Mtandao wa Wadau wa kupambana na unywaji pombe kupita
kiasi – TAAnet unaungana na wadau wote Nchini na Duniani kote kupinga
matumizi ya pombe. TAAnet inaunga mapendelezo ambayo yamefanyiwa tafiiti
na kupendekezwa na Shirika la Afya Dunuani mwezi Septemba mwaka huu
katika repoti yake ya Global status report on alcohol and health
2018.
WHO inapendekeza kuwa ila kuweza kuzia madhara
yote yanayotokana na matumizi mabaya ya pombe kunahitajika uwezo
mkubwa na ujuzi wa kisayansi kwa watunga sera juu ya ufanisi wa mikakati
yafuatayo:
- Kudhibiti uuzaji wa vinywaji holela (hasa kwa vijana), pamoja na kusimamia na kuzuia upatikanaji wa pombe;
- Kufanya maboresho ya sheria ya usalama barabarani na kutengeneza sera ili kuthibiti madereva wanaoendesha gari huku wakiwa wamelewa;
- Kupunguza mahitaji kupitia kodi na taratibu za bei;
- Kuzidi kutoa elimu ya ufahamu wa matatizo ya afya yanayosababishwa na matumizi mabaya ya pombe na kusimamia utekelezaji sera ;
- Kurahisisha upatikanaji na matibabu ya gharama nafuu kwa watu wenye matatizo ya matumizi ya pombe; na
- Kuzuia matangazo katika vyombo vya habari yanayohamasisha kuhusu matumizi ya pombe.
Sisi Wadau wa mtandao tuna amini kuwa Sera
zenye ufanisi na utekelezaji ni muhimu kwa kupunguza madhara yanayosababishwa
na pombe Tanzania.
Kama wadau wa kupambana na madhara ya unywaji
pombe , tungependa kuona watunga sera wanalitafutia tatizo hili suluhisho
kwa kuja na ufumbuzi wenye ubunifu ambao utaokoa maisha ya watu, kama
vile kutokomeza unywaji pombe kupindukia.
Tanzania ni miongoni mwa Nchi ambazo bado haina
sera/muongozo wa pombe ukilingalinisha na Nchi jirani kama Zambia, Kenya,
Malawi huku Uganda wakiwa njiani kumalizia mkakati wa sera yao ya pombe.
TAAnet inapendekeza kupitiwa kwa sheria na
kuweka masharti kuhusiana na matangazo, uuzaji na udhamini wa pombe pamoja na
kuonyeshwa kwa onyo la athari za pombe kwenye matangazo ya vilevi
ili kupunguza matumizi yake kwa jamii.
TAAnet inaamini kwamba, endapo kutakuwa na sera
ya kudhibiti matumizi mabaya ya pombe, wanaume watawajibika zaidi na kuacha
matumizi ya vileo yaliyopitiza , yanayochangia unyanyasaji wa kijinsia, na
badala yake kuchangia ustawi wa familia na kukuza maendeleo kwenye jamii na
katika Taifa kwa ujumla.
Kupunguza matumizi mabaya ya pombe kutasaidia
kufikia malengo ya Malengo endelevu ya dunia (SDGs) yanayohusiana na afya ikiwa ni pamoja na afya ya uzazi na
watoto, magonjwa ya kuambukiza, magonjwa yasiyoambukizwa na magonjwa ya akili,
majeraha na sumu.
Ni wakati muafaka kwa sasa kwa Serikali, wanasiasa na watunga
sera kuchukua ajenda hii na kuifanyia kazi katika mipango kazi zao
mbalimbali.
Kwa taarifa hii kama ilivyotolewa kwa niaba ya Mtandao wa Asasi zinazopinga
matumizi mabaya ya pombe nchini Tanzania, naomba kuwasilisha.
Sophia
Komba
Mwenyekiti
- TAAnet